LUGHA ni chombo muhimu cha mawasiliano na ni daraja la kufikisha na kueneza maarifa miongoni mwa wanajamii.
Katika kutambua ukweli kuhusu lugha kama chombo muhimu cha kuunda fikra miongoni mwa wanajamii, lugha ya taifa ilitumika kupiga vita ukabila.
Zamani mataifa mengi ya Afrika yalikuwa yakitumia lugha za asili (makabila) sambamba na lugha za kikoloni, mfano Kifaransa, Kiingereza na Kireno.
Mtihani kwa wapigania uhuru ukawa ni juu ya lugha gani hasa itumike  kama lugha rasmi ya  mataifa yao.
Tofauti na mataifa mengine ya Afrika, Tanzania tulikuwa na lugha yetu adhimu ya kiasili ambayo haikuwa na mfungamano  na kabila lolote katika nchi yetu.
Ni kwa sababu hizi ndiyo maana waasisi wa taifa letu kwa busara na hekima wakaamua kuifanya lugha  hii kuwa lugha ya taifa na ya kufundishia elimu ya awali, msingi, mafunzo ya cheti cha elimu ya ualimu na elimu ya watu wazima.
Sambamba na Kiswahili, Kiingereza kikapitishwa kuwa lugha rasmi ya shughuli zote za kiserikali na kufundishia kwa ngazi ya elimu ya sekondari na vyuo vikuu vyote nchini.
Matumizi ya Kiingereza serikalini na katika elimu ya juu  nchini  yalichangiwa na uchache wa wataalamu wazalendo, hivyo kulazimika kutumia wataalamu wengi wa kigeni.
Lakini kwa utashi wa viongozi wetu wa Serikali ya Awamu ya Kwanza, juhudi na mipango madhubuti ikawekwa ili kuikuza na kuistawisha  lugha  ya Kiswahili ndipo taasisi  mbalimbali kama vile  BAKITA, UKUTA na Taasisi  ya Uchunguzi wa Kiswahili ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam  (TUKI hivi sasa TATAKI)  zilianzishwa ili kulifikia lengo hilo.
Na hivi sasa ukweli unadhihirika kuwa Kiswahili ni lugha inayojitosheleza kimisamiati na imeendelea kukua na kukubalika kimataifa.
Hili linathibitishwa na namna vyuo vikuu mbalimbali duniani vimekuwa vikifanya jitihada za kufundisha lugha hii.
Kiswahili kinafundishwa katika vyuo vikuu kama Havard, Yale, Stanford, Princeton, Chuo Kikuu cha Pennsylvania na vinginenyo.
Inakadiriwa nchini Marekani peke yake kuna taasisi karibu 100  zinazojihusisha na ufundishaji wa Kiswahili. Pia vituo mbalimbali vya  redio duniani vinarusha matangazo yake  kwa Kiswahili kupitia idhaa za Kiswahili za BBC, DW, RFI na VOA.
Hadi sasa  ukweli uko wazi hususan kwa Watanzania kuwa Kiswahili si lugha muhimu kwetu bali ni  lulu ambayo hatuna budi kuikuza, kuiendeleza,  kuilinda, kuisambaza na kuipigania kwa hali na mali katika nyakati hizi ambazo kila taifa hususan mataifa tajiri yakiendelea kuzisambaza lugha zao.
Kwa Watanzania, Kiswahili kina umuhimu mkubwa sana si tu kwa  mwananchi  mmoja mmoja bali hata kwa taifa  kwa ujumla.
Kiswahili ni silaha ya ukombozi wa kijamii, katika uwezo huu tu ndipo mtu anakuwa na uwezo wa kutoa  mchango wake katika ujenzi wa taifa lake.
Mwanazuoni nguli wa Afrika, Profesa Ngungi wa Thiong’o,  akizungumza katika Mhadhara wa Kitaaluma katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kabla ya chuo hicho kumtunuku shahada ya heshima ya udaktari katika fasihi mwishoni mwa mwaka 2013, alisema: “Lugha ni  silaha ya kivita baina ya mtumwa na mtawala; ni silaha ya kutamalaki kama ilivyo upanga, lakini Waafrika wengi kwa  kulowea  upumbavu wa usasa, tumeziweka lugha zetu za asili kwenye uduni na kutukuza za kigeni kana kwamba  ni kinyaa  kuzungumza za kwetu,  huku ni kumezwa na hakuna wa kukwepa kwamba tuko mateka.
“Kuna wasomi wajinga, wanaodhani kuzungumza lugha zao  mfano Kiswahili ni kujidhalilisha, hivi ni nani alikufa kwa kuzungumza Kiswahili na nani akahesabiwa haki ya kuishi kwa kuzungumza Kiingereza?
Si viongozi wa serikali za Afrika pekee waliotekwa na  fikra za kigeni, bali hata wasomi wa karne ya sasa ni majemedari wanaopigana vita upande wa adui.
Majemedari hao tena  wakiwa na majina ya Kizungu  na kuweka kando  ya asili.
“Wanaona fahari kutumia lugha za kigeni kama silaha ya maendeleo, bila kujua kuwa  wanaangamizwa wao na vizazi vyao na kuendelea kujenga  matabaka makubwa.”
Anasema Tanzania  ndiyo nchi pekee inayotumia Kiswahili kama lugha yake ya taifa. Hivyo kwa kuikuza na kuiboresha  kwa kuitumia katika shughuli zote  za kiserikali na kielimu itakuwa njia nzuri ya kuendelea kulitangaza taifa letu kimataifa.
Ukweli ni kwamba Kiingereza  kinachangia kudorora kwa elimu nchini. Kwa shule chache nilizopita na kufundisha katika mikoa ya Lindi, Dar es Salaam,  Iringa, Mbeya na Kigoma kilichopo kinatisha.
Si zaidi ya asilimia kumi ya wanafunzi darasani  utakuta ndio wana uwezo  wa kuandika sentensi ya Kiingereza iliyonyooka na yenye maana. Katika hali kama hii inakuwa kazi kufanya vema katika masomo yao, wanaishia kusoma kwa kukariri na wakati mwingine hata wasiweze  kuvioanisha  vitu wanavyojifunza  na mazingira yao halisi ya kimaisha.
Mwanafunzi anayejifunza elimu ya awali  (mwaka mmoja au miwili) na elimu ya msingi  (miaka  saba) kwa Kiswahili, kumfundisha kwa Kiingereza tupu  katika elimu ya sekondari  ni kumpa mtihani wa kuanza kujifunza  lugha mpya na kuishia kukariri bila kuelewa kwa mapana yale anayojifunza darasani.
Ni katika mfumo huu ndio tunazalisha mawaziri wa elimu  wasioweza kujieleza kwa Kiingereza, madaktari wanaofanya upasuaji na kuacha mikasi tumboni mwa wagonjwa, madaktari wanaotakiwa kupasua mguu wanapasua kichwa na kuleta maafa na kupunguza nguvu kazi ya taifa. Haya yote ni matokeo ya kuipuuza lugha yetu ya thamani.
Umoja na amani tunayoishuhudia  nchini mwetu pamoja na sababu nyingine ni kutokana na lugha hii  kuweza kutuunganisha  watu wa  makabila tofauti, hali  inayochangia kuendeleza utengamano wa kitaifa  na hii inatoa hamasa na chachu  katika  harakati  za  kulinganisha Bara la Afrika na kuunda taifa moja la Afrika.
Kiswahili pia kina uwezo wa kulinda afya ya Watanzania kwa sababu vipodozi vingi kutoka nje, maji na vyakula vya viwandani huwekwa vibandiko vya maelekezo kwa watumiaji  vilivyoandikwa kwa Kiingereza.
Katika muktadha  wa sasa si zaidi ya asilimia 10 ya Watanzania ndio wanaojua kuongea Kiingereza kwa ufasaha.
Matumizi ya vyakula, maji na vipodozi vilivyoandikwa maelekezo ya matumizi yake kwa lugha za kigeni  ni hatari kwa afya za wananchi. Hivyo matumizi ya Kiswahili ni njia pekee  ya kukabiliana na tatizo hili.
Kuna tatizo gani kwa wazalishaji wa viwandani hususan wa vile viwanda vya ndani  kushinikizwa kuweka  maelekezo ya matumizi ya bidhaa  kwa lugha ya Kiswahili?
Matumizi ya Kiswahili yanaweza kulinda masilahi ya taifa katika mikataba ya kimataifa  hususan ile inayohusiana na rasilimali za nchi na  mambo ya usalama.
Mikataba mingi ya kimataifa inaandikwa katika lugha  ngumu za  kisheria, hivyo wakati fulani inaweza kuwayumbisha wataalamu wanaohusika na kusaini mkataba husika.
Historia inatufunza na kutukumbusha  kuwa moja ya sababu iliyosababisha sehemu kubwa ya Bara la Afrika kutawaliwa na ukoloni kwa  karibu karne nzima ilitokana na viongozi wa jamii za Kiafrika kusaini mikataba  wasiyoijua.
Pamoja na hilo, umma wa Watanzania ambao hawajui lugha za kigeni unanyimwa fursa ya kuijua  mikataba hiyo na namna inavyoweza  kuwanufaisha.
Miongoni mwa  vitu  vinavyodhalilisha utu  wa mtu ni pamoja na  kukumbatia  tamaduni za  kigeni, mfano  kuchapa viboko  na kuwapa  vijana wetu waliopo mashuleni adhabu  nzito  kwa sababu  tu wameongea Kiswahili. Huu ni utumwa mamboleo.
Ni vema tukaukomesha.  Ni aibu kuendelea kuchapana  wenyewe kwa wenyewe  kwa sababu ya lugha za kigeni kama Wazungu na Waarabu  walivyowachapa babu na bibi zetu enzi za utumwa.
Umewaona  Wazungu wakichapa vijana wao kisa  hawaongei lugha za Kiafrika?  Mbona Wachina, Waarabu,  Wajapani, Warusi na wengine hawawachapi vijana wao kwa sababu  ya  kutojua kuongea  Kiingereza au Kifaransa? Hii ni aibu tunayowajibika kuifuta mara moja.
Isitoshe  viboko na adhabu nyingi zinawajengea hofu wanafunzi hatimaye  kufanya vibaya katika masomo yao.
Sheria na miswada mingi ya sheria serikalini inaandaliwa na  kuhifadhiwa kwa Kiingereza. Watawala wanalifanya hili huku wakijua kuwa zaidi ya asilimia 80 ya Watanzania  hawajui Kiingereza.
Kama ilivyotokea wakati wa kuandaa muswada wa sheria ya mabadiliko ya katiba mwaka 2011; hadi pale wananchi kupitia vyama vya upinzani na taasisi za kiraia kutoa shinikizo, ndipo watawala wakakubali kuubadili muswada ule na kuuandika kwa Kiswahili.
Hapa lengo ni kuwanyima  fursa Watanzania kujua taarifa za msingi zinazohusiana na taifa lao.  Tunaomba Katiba Mpya itamke  kuwa Kiswahili ni lugha ya taifa itakayotumika  katika mawasiliano yote serikalini na kufundishia shule za awali hadi vyuo vikuu.
Kwa kuidhinisha  Kiswahili kutumika katika ngazi zote za elimu kuna fursa za ajira kupatikana kwa Watanzania kupitia kampuni  za vitabu  za ndani ya nchi kwa kuongeza  wigo wa soko, hivyo mapato yao yataongezeka na kupanua fursa za ajira kwa kampuni zao na wataalamu wa  kutafsiri vitabu vya kigeni watahitajika kwa wingi zaidi.
Pamoja na umuhimu wa lugha hii kwa upande wa mwananchi mmoja mmoja bado kuna watu wenye hoja za kupinga, baadhi  wanasema  Kiswahili hakina misamiati  ya kutosha hivyo hakifai kufundishia elimu  ya  sekondari na vyuo vikuu.
Wenye mawazo haya  wanachoshindwa kufahamu ni kuwa kadiri lugha inavyotumika ndivyo inavyoendelea kukua  na misamiati yake  kuongezeka na kadiri lugha isiyotumika ndivyo inavyoendelea kudumaa na hatimaye kutoweka kabisa.
Na  katika  kudhihirisha kuwa  misamiati si tatizo  katika Kiswahili;  kampuni ya kuchapa vitabu  ya Mkuki  na Nyoka kwa kushirikiana na Haki Elimu  wamezindua kitabu  cha kemia  kwa elimu ya sekondari kilichoandikwa kwa Kiswahili kinaitwa  ‘Furahia Kemia’  ambacho kimeandikwa na jopo la walimu wa Tanzania.
Taasisi na wataalamu  mbalimbali wamesema masomo yote yakiwemo ya sayansi yanaweza kuandikwa kwa Kiswahili.
Wengine wanasema mbona hata somo la Kiswahili wanafunzi wanafeli, sasa kama hoja  ni kuboresha elimu  hata tukitumia Kiswahili wanafunzi  wataendelea  kufeli tu, wanafunzi wanafeli Kiswahili kutokana na kutokuwa  na mipango madhubuti ya kuongeza hamasa kwa wanafunzi kupenda na kusoma kwa bidii  lugha yao ya taifa.
Wapo wanaosema kuwa Kiingereza ni Kiswahili cha dunia hivyo katika nyakati hizi za utandawazi ni sharti tuijue lugha hiyo inayozungumzwa na watu  wengi duniani.
Wabebaji  wa hoja   hii wanapaswa kufahamu jambo moja kuwa utandawazi si lugha bali utandawazi ni  ujuzi na maarifa.
Hivyo ili kuwa na jamii yenye uwezo wa kushindana katika zama hizi za utandawazi ni sharti kuwa na jamii yenye ujuzi na maarifa ya hali ya juu yanayopatikana kwa vijana kufundishwa kwa lugha inayoeleweka vema kwa mfundishaji na mfundishwaji.
Tuelewe kwamba Kiingereza  na lugha zingine za kigeni zinazofundishwa shuleni na vyuoni zitaendelea  kufundishwa kama somo huku masomo  yote  mengine yakifundishwa kwa lugha ya Kiswahili.
Mfano nchi ya Italia  pamoja na kufundisha kwa lugha yao ya asili lakini zaidi ya asilimia  34 ya wananchi wake wanaweza kuongea Kiingereza, kwa Israel wao ni asilimia 84, Ujerumani 56,  Ufaransa 39, Hispania 22 na Uholanzi asilimia 90.
Tanzania pamoja na kufundisha kwa Kiingereza  masomo yote  kwa zaidi ya nusu karne  tokea tupate uhuru idadi ya wazungumzaji wa lugha hiyo hawazidi asilimia 10 (wanaojua kuongea na kuandika Kiingereza fasaha si kiswanglishi).
Ni kwa kutumia lugha zao ndiko kulikoifanya China, Japan, Ujerumani, Urusi na mataifa yote makubwa duniani kuboresha elimu zao na hatimaye kuweza kutoa wasomi waliobobea na kupiga hatua kubwa kiteknolojia na kiuchumi

src
Tanzania Daima

0 comments:

Post a Comment

 
Top