Viongozi wa UKAWA

            DEMOKRASI yetu ni ya aina gani kama hatuamini katika kupewa nafasi kwa mawazo ya wengi. Demokrasia hii ni ya aina yake ambapo wachache hatuna uvumilivu pale inapothibitika kuwa wapinzani wetu wametuzidi kwa wingi unaotokana na uchaguzi za kidemokrasia na hivyo wanahaki ya kupitisha wanachoamini? Msingi mmoja muhimu wa demokrasia ni kukubali mawazo ya wengi. Usahihi wa hoja mara nyingi sio jambo muhimu kuliko wingi wa ufuasi. Msingi mwingine muhimu wa demokrasia ni utawala wa sheria. Ni uelewa wangu huo wa demokrasia unaonishawishi nisikubaliane na mantiki ya msimamo wa kundi linalojiita Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA) lililoamua kususia Bunge la Katiba wiki iliyopita. Chama cha Mapinduzi (CCM) kina wajumbe wengi katika Bunge la Katiba. Msingi wa wingi wao ni ushindi walioupata katika uchaguzi halali wa kisheria na kidemokrasia. UKAWA wanalijua hilo na hawawezi kuhoji uhalali wa Bunge hilo sasa, baada ya kuingia bungeni na kuanza kushiriki maana maji ukiyavulia nguo, sharti uyaoge. Kadhalika, ni dhahiri kuwa UKAWA hawabishi kwamba Bunge la Katiba lina uwezo wa kubadili vifungu katika rasimu kama mabadiliko hayo yanaungwa mkono na wabunge wengi. Hata hivyo, ni jambo la ajabu kuwa UKAWA hawataki CCM watumie wingi wao kubadili vifungu hivyo. CCM walipofanya hivyo, UKAWA wakalalamika kuwa CCM wamepindua rasimu na kupuuza maoni ya wananchi. Lakini, kwa kufanya hivyo je, CCM wanakiuka sheria? Ni dhahiri kuwa CCM wana uhalali wa kisheria kubadili vifungu vya rasimu. Akilijua hili, Zitto Kabwe aliandika katika akaunti yake ya mtandao wa kijamii wa Facebook: “Majadiliano ya upande mmoja yanaweza kuwa halali kisheria (legal legitimacy) lakini yanakosa uhalali wa kisiasa (political legitimacy)”. Katika nukuu hiyo ambapo Zitto anasema huenda upo uhalali wa kisheria, kwa upande mwingine anatilia shaka uhalali wa kisiasa. Hata hivyo, uhalali wa kisiasa utakosekana vipi kama hakuna hoja nzito zinazohalalisha ususiaji? Kimsingi, kwa mujibu wa Ismail Jussa, sababu tatu za uamuzi wa UKAWA kususia Bunge aliouita uamuzi wa hekima na busara ni pamoja na kile alichoita CCM kupindua Rasimu ya Katiba ya Wananchi na kupenyeza rasimu yao yenye lengo la kuwalinda watawala na mafisadi. Kwamba, kinachopendekezwa na CCM ni rasimu ya kuwalinda mafisadi, ni maoni ya UKAWA lakini je, sheria inawakataza kubadili vifungu vya rasimu vile waonavyo kama wana wingi wa wajumbe? Sababu ya pili ya UKAWA ya kutoka bungeni ni Waziri William Lukuvi kutumia kanisa kupandikiza chuki na kuchochea vurugu kwa kurejea kauli ya Rais Jakaya Kikwete, kwamba ukipitishwa muundo wa Muungano wa Shirikisho la Serikali tatu, jeshi litachukua madaraka na kwamba Zanzibar itaunda dola ya Kiislamu dhidi ya Wakristo. Lukuvi kama alifanya hivyo bila shaka alikosea. Lakini Lukuvi ni mmoja kati ya wajumbe wengi wa Bunge la Katiba na wala si mwenyekiti au kiongozi wa Bunge hilo. Pili, hatua sahihi ilikuwa ni kupeleka malalamiko rasmi kwa uongozi wa Bunge hilo na mamlaka iliyomteua kuwa Waziri. Vinginevyo, kama kila matamshi ya uchochezi yakitumika kuhalalalisha kususa, hakuna shughuli zinazoweza kuendelea mbele. Lakini Profesa Ibrahim Lipumba ambaye analamlalamikia Lukuvi naye hayuko nyuma katika siasa za misikitini. Siku mbili baada ya kususia Bunge, video ikawekwa Facebook ikimuonyesha Profesa Lipumba akihutubia Waislam msikitini. Yaliyomo humo sitaki kuyataja hapa au kuyatafsiri. Sababu ya tatu iliyosukuma UKAWA kususia Bunge la Katiba ni kile walichodai kuwa mjadala wa Bunge la Katiba umegeuzwa jukwaa la kuhubiri matusi, chuki, ubaguzi wa rangi na ukabila. Kama UKAWA wanakimbia kauli za ubaguzi, wanadhani wapi na lini watapata jukwaa lao peke yao kuzungumza? UKAWA walipaswa kuendesha mapambano yao dhidi ya kauli za ubaguzi ndani ya Bunge, na sio nje. Mikutano watakayoifanya na wananchi haitowabadili wajumbe wa CCM katika Bunge la Katiba na baada ya kumaliza mihangaiko yao, wakirudi watawakuta wenzao vile vile. Kutokana na mazingira haya, mjadala wa upande mmoja utakaoendelea bungeni ni halali, hata kama UKAWA wakiendelea kususia. Kwa maoni yangu, uamuzi wa UKAWA wa kususia Bunge sio wa busara kabisa. Katika siasa za ushindani unaweza kushinda au kushindwa. Kama ambavyo UKAWA wanaamini sana katika Serikali tatu, wapo wengine wanaoamini sana katika Serikali mbili au moja na tupo baadhi ambao hatuutaki hata huo Muungano. Lakini haiwezekani mifumo yote mitatu itumike ndio maana kila upande unapong’ang’ania msimamo, mnapiga kura za kuamua. Dhana kuwa CCM hawana hoja nayo haina mashiko. Tumeshuhudia hata miongoni mwa jamii ya wasomi, wanaoangalia mambo kwa ushahidi wa kitaaluma, baadhi wakiunga mkono Serikali mbili, sembuse wanasiasa ambao hawatumii vipimo vya kisomi katika kujenga hoja? Bila upendeleo, mtu yeyote anayetumia vigezo vya kitaaluma ni rahisi kutilia shaka takwimu za Tume ya Katiba kama kweli zinathibitisha kuwa wengi wanataka Serikali tatu. Hili limezungumzwa sana, na ni bahati mbaya kuwa UKAWA wanajaribu kuonyesha kuwa ukosoaji huu ni kumdharau Jaji Joseph Warioba na tume yake iliyojaa baadhi ya watu wenye heshima kubwa ndani na nje ya nchi. Kwa upande mwingine, hata bila ya hoja za Serikali mbili, Muungano wa UKAWA ni rahisi kumtisha mtu yeyote kwa sababu kinachowaunganisha watu wa UKAWA ni upinzani dhidi ya Serikali mbili tu. Ukiacha hilo, kila moja katika kundi la UKAWA linahitaji mfumo tofauti, baadhi wakidai Muungano wa mkataba, wengine wakidai Serikali tatu za marais watatu na wengine wakidai Serikali tatu chini ya rais mmoja na mawaziri wakuu wawili. Kadhalika, wote tunajua historia ya minyukano kati ya vyama vinavyounda UKAWA hususan CUF na CHADEMA. Binafsi, sina imani na UKAWA kwa sababu ni muungano wa maslahi ya muda mfupi ambao huenda zikikubalika Serikali tatu tusishangae kukaibuka UKAWA- asili na UKAWA - mpya! Hata hivyo vyovyote iwavyo, kwa maslahi ya demokrasia na utawala wa sheria, UKAWA wanapaswa warudi bungeni wakaendelee kupambana. Wakishindwa tutasema wamekufa kiume ingawa demokrasia na utawala wa sheria vimefuata mkondo wake. Kabla ya kurudi bungeni, UKAWA wanapaswa kujipanga vizuri zaidi kwa hoja, walifanya makosa kadhaa ikiwemo kung’ang’ania hoja ya uhalali wa Muungano, ambayo haina maana yoyote na ilisukuma kutajwa kwa udhaifu wa watu wanaochukuliwa kama nembo ya taifa hili, Mwalimu Julius Nyerere na Abeid Aman Karume. Halikuwa jambo zuri kuhoji uhalali wa Muungano wenyewe na waliyoyafanya waasisi hao katika miongoni mwa taratibu za kuunganisha nchi hizi kwa sababu wazee hao waliishi katika zama tofauti, tena wakiendesha taifa changa. Kama walifanya makosa ya makaratasi na vikao, hayawezi kuharamisha Muungano tuliouishi miaka 50 sasa. CCM hawawezi kuwapa UKAWA Serikali tatu. Lakini upo uwezekano wa kuandaa kura ya maoni ili wananchi wapate nafasi ya moja kwa moja ya kusema wanautaka au hawautaki Muungano na kama wanautaka uwe wa mfumo gani. Hiyo ndio hoja ambayo UKAWA wanapaswa kuisimamia. Hilo likipita hakuna mshindi wa moja kwa moja, lakini utatuzi wa kudumu wa mfumo wa Muungano utapatikana. Wazo la kura ya maoni likikataliwa, bado UKAWA wanayo nafasi ya kushawishi wananchi waikatae Katiba katika kura ya maoni. Kadhalika, Uchaguzi Mkuu ni mwakani tu, wajipange na kwa kuwa kama wanavyojinasibu wao ndio wawakilishi wa wananchi, watashinda na kuanzisha mchakato mwingine wa uuundaji

src
Raia mwema
Njonjo Mfaume

0 comments:

Post a Comment

 
Top