TAIFA liko kwenye mjadala mkubwa wa kijamii na kisiasa katika mchakato muhimu wa kuandika upya Katiba.
Mchakato huu umetokana na malalamiko kutoka kwa watu kadhaa kuwa Katiba, ambayo imelilea Taifa tangu mwaka 1962, imezeeka, imejaa viraka na hivyo iandikwe upya.
Baada ya kauli ya Rais Jakaya Kikwete ya Desemba mwaka 2011 kwamba angeanzisha mchakato wa kuandika upya Katiba, Bunge lilitunga Sheria ya Mabadiliko ya Katiba, sura 83 mwaka 2012 na mchakato ukaanza kwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba kukusanya maoni na kuwasilisha Rasimu ya pili ya Katiba bungeni mapema Machi, 2014.
Bunge Maalumu la Katiba sasa linaendelea na vikao vyake Dodoma. Mjadala mkali umezuka na unaedelea, kuhusu muundo wa serikali baada ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba kupendekeza kuundwa kwa shirikisho la serikali tatu, kinyume na Katiba ya sasa (Katiba ya mwaka 1977) yenye serkiali mbili.
Je, Katiba yetu imezeeka na hairekebishiki?
Japo swali hili halina umuhimu tena kwa sasa kwani mchakato wa kuandika Katiba mpya unaendelea, mazingira na mijadala inavyoendelea inalazimu wadadisi kurejea swali hili.
Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania iliandikwa mwaka 1977, miaka 37 iliyopita. Tangu wakati huo, imefanyiwa marekebisho kwa nyakati na sababu tofauti mara 14. Katiba hii iliandikwa baada ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar mwaka 1964 ambapo ilikubaliwa kwamba Katiba ya Jamhuri ya Tanganyika ya mwaka 1962 ifanyiwe marekebisho ili kuipa sura ya Muungano na kuifanya kuwa Katiba ya Mpito.
Marekebisho hayo yalifanyika mwaka 1965 na hivyo kuifanya Katiba ya mpito hadi mwaka 1977 ilipoandikwa Katiba ya Kudumu inayotumika hadi hivi sasa.
Tanzania, ambalo ni Taifa la Muungano wa Nchi Mbili za Tanganyika na Zanzibar, ni Taifa changa kwani lina umri wa miaka 50 tu. Ziko nchi zenye umri zaidi ya Taifa letu ambazo zimeendelea kutumia na kurekebisha katiba zao.
Marekani, kwa mfano, inatumia katiba yenye umri wa zaidi ya miaka 200 na ambayo imefanyiwa marekebisho zaidi ya mara 100.
India, kwa upande wake, iliandika katiba yake ya Uhuru mwaka 1945, miaka 70 iliyopita, mwaka 2012 iliifanyia marekebisho katiba yake, marekebisho ya 94 Katika yake hiyo ya mwaka 1945.
Hivyo, madai kwamba Katiba yetu ya sasa imezeeka na kujaa viraka (kwa kufanyiwa marekebisho mara 14) na hivyo iandikwe mpya ni madai yanayoacha mjadala.
Msingi wa malalamiko kuhusu Katiba ya sasa (ya Mwaka 1977)
Kwa mujibu wa taarifa na nyaraka mbalimbali zilizoambatishwa na Rasimu ya pili ya Katiba ‘mpya’ iliyowasilishwa bungeni na Jaji Warioba, Machi 2014, madai ya kuandikwa upya kwa Katiba yetu ni kwamba;
Muungano, ambao umedumu kwa mika 50 sasa, umeghubikwa na malalamiko mengi kutoka kila upande, hasa Zanzibar kulalamika kwamba Tanzania Bara, inanufaika zaidi kiuchumi kwa kuwa Serikali ya Tanzania Bara ndiyo hiyo hiyo ya Muungano wa Tanzania, na hivyo, Bara ‘kuvaa koti la Muungano’.
Madai hayo ya Zanzibar, yameufanya upande huo wa Muungano kuwa na majaribio na maombi ya mara kwa mara ya kudai ‘uhuru zaidi’, hasa kwa lengo la upande huo kunufaika zaidi kiuchumi na kijamii na mahusiano ‘ya nje’.
Kwa upande wa Bara, malalamiko machache yaliyopo ni kwamba ‘upande wa Zanzibar unanufaika zaidi na fursa na faida za Muungano’, wakati huo huo, kutokana na mazingira yake (ya udogo kieneo na kwa idadi ya watu), Zanzibar kuchangia kidogo au kutochangia kabisa ‘gharama za Muungano’.
Mabadiliko ya Kisiasa na Kijamii ambapo Katiba ya sasa, licha ya kufanyiwa mabadiliko, kwa mfano, mwaka 1992 kuruhusu Mfumo wa Vyama vingi, bado Katiba imekuwa ni kikwazo kwa vyama vya siasa vya Upinzani kufanya vizuri katika chaguzi kwa madai kwamba Tume ya Uchaguzi, na vyombo vingine vya demokrasia vimebanwa kikatiba kuegemea upande wa chama tawala hasa kwa kuwa viongozi wake wanateuliwa na Rais ambaye ndiye kiongozi wa chama tawala.
Kuwepo kwa umasikini mkubwa miongoni mwa Watanzania, umasikini ambao hauendani na utajiri wa Taifa wa Maliasili; hali inayoashiria kwamba Katiba ya Sasa haijaweka mifumo mizuri ya kusaidia wananchi wanufaike na kuendelezwa na maliasili na utajiri wa asili wa Taifa letu.
Hali hii imeelezewa kusababishwa na mifumo dhaifu ya uwajibikaji wa viongozi; kukoseka kwa dira ya Taifa baada ya Azimio la Arusha kufutwa mwaka 1991 na misingi dhaifu ya Haki za Binadamu.
Ukweli na uhalali wa sababu au madai ya Katiba mpya na jinsi madai hayo yalivyozingatiwa Katika Rasimu ya Pili ya Katiba inayojadiliwa bungeni.
Kama ilivyoelezwa, msingi mmojawapo wa sababu za kuandika upya kwa Katiba ni malalamiko kuhusu ‘manufaa, hasa ya kiuchumi na kijamii’ ya Muungano.
Nitalizungumzia zaidi eneo hili kwa sasa, na maeneo mengine ya ‘uhuru wa tume ya uchaguzi na vyombo vingine vya kukuza demokrasia’ pamoja na eneo la ‘udhibiti na usimamizi wa rasilimali za Taifa kwa manufaa ya wananchi’, nitayazungumzia katika makala zitakazofuata.
Muungano wa Tanzania, na hasa muundo wake, limekuwa ni eneo la mjadala mpana na mkali sana wakati huu wa mjadala wa Rasimu ya Pili kwenye Bunge Maalumu na nje ya Bunge.
Kwa kutambua umuhimu wa Muungano, Bunge la Jamhuri ya Muungano, lilipopitisha Sheria ya Mabadiiko ya Katiba, sura 83, katika kifungu 9(2), liliweka maeneo ambayo yanapaswa kulindwa na kuzingatiwa katika Mchakato na hatimaye kuandikwa kwa Katiba mpya.
Kati ya maeneo hayo, ni uwepo wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.
Katika kufanya kazi yake, Tume ya Mabadiliko ya Katiba, ilizingatia eneo hilo kwa mtazamo kwamba ‘eneo hilo linapaswa kulindwa na kuimarishwa’, na hivyo tume kujipa uhuru wa ‘kupendekeza marekebisho’ ambayo Tume inaamini yataboresha Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Kwa utafiti wa aina za Muungano, Tume inasema, Muungano wa nchi zaidi ya moja huleta ama serikali moja (yaani Muungano uitwao unitary union), au serikali mbili au zaidi (katika mfumo wa shirikisho, yaani federation) au serikali tatu zinazoshirikiana kimkataba (yaani confederation).
Katika aina zote hizo za muungano, bado uwezekano wa muungano kuvunjika upo (bila kujali idadi ya serikali zinazoundwa baada ya muungano).
Kwa maoni ya Tume, uimara wa muungano hautokani na idadi ya serikali zinazoundwa, bali ‘dhamira ya kisiasa’ kusimamia na kumaliza ‘malalamiko kuhusu muungano yanayotoka kwenye nchi washirika’.
Kwa tafsiri hiyo ya kifungu hicho cha sheria, Tume, kwa kuamini kwamba inaboresha na kwa kuzingatia tafiti kadhaa ambazo ilifanya na kwa kusikiliza maoni ya wananchi kadhaa kuhusu jambo hilo (la Muungano) na kwa kutambua hatua ambazo zimekuwa zikichukuliwa na upande mmoja wa Muungano, hususan Zanzibar kujitafutia ‘uhuru zaidi’ (hasa kupitia marekebisho ya 10 ya Katiba ya Zanzibar ya Mwaka 1984 yaliyofanywa mwaka 2010) , ilipendekeza ‘kuivua Tanzania Bara koti la Muungano’, na hivyo kupendekeza kuwepo kwa serikali ya ‘kati au ya Ushirika au ya Washirika wote wawili’, serikali ya Tatu, ya Shirikisho, sambamba na ile ya Tanganyika inayoanzishwa kutoka Tanzania Bara iliyokuwa ndani ya Muungano.
Utafiti wa tume kwa nchi mbalimbali zilizoungana, unaonyesha kwamba, ipo miungano iliyodumu ya serikali moja, na mingine ya serikali mbili au zaidi (yaani ya shirikisho), na pia ipo mifano ya nchi zilizokuwa za muungano zilizokuwa za serikali moja na nyingine zaidi ya serikali mbili ambazo miungano yao imevunjika.
Hii inathibitisha ukweli kwamba, idadi ya serikali pekee, hailindi muungano. Nchi za Somalia (Somalia na Somaliland); Ethiopia (Ethiopia na Eritrea), Sudan (Sudan Kusini na Kaskazini) zote zilikuwa na muungano wa serikali moja (unitary union), lakini miungano hiyo imevunjika.
Zipo pia nchi za shirikisho, kama Urusi (USSR), Chekoslovakia na Yugoslavia zilizokuwa za shirikisho nazo zimesambaratika! Aidha, zipo nchi zenye mashirikisho (serikali zaidi ya moja) ambazo zinaendelea kudumu kama vile Canada, India, Brazil, Marekani na hata Ujerumani.
Kwa hiyo, kwa maoni ya Tume, dawa ya kulinda muungano wetu ni kubadilisha muundo wa muungano huo kutoka muundo wa serikali mbili wenye malalamiko lukuki yasiyokoma, na kuunda shirikisho la serikali tatu ambazo mipaka yake ya kiutendaji inaeleweka vizuri.
Kwa mtazamo wa Tume na baadhi ya watu, kuitenganisha Serikali ya Tanganyika na Serikali ya Muungano, kutapunguza malalamiko, hasa kutoka upande wa Zanzibar kwamba Tanganyika imevaa koti la Muungano na hivyo kunufaika zaidi kiuchumi na Muungano.
Malalamiko ya Zanzibar, ambayo yamekuwa kichocheo kwa mshirika huyo katika Muungano kuchukua hatua za ‘kujitafutia uhuru zaidi’ na hivyo kunufaika zaidi kiuchumi, yasiporekebishwa yanaweza kusababisha Muungano kuvunjika, jambo ambalo Tume imeagizwa kisheria kwamba iweke mazingira ya kuzuia lisitokee.
Hali ya Muungano ikoje kwa sasa, nani ananufaika zaidi?
Ukiuliza swali hili kwa kila upande wa Muungano, kila upande utasema upande mmoja unanufaika zaidi. Tuanze na upande mmoja baada ya mwingine.
Upande wa Zanzibar unatuhumu Bara kunufaika zaidi hasa kwa misingi ifuatayo:-
Tanzania Bara, ambayo iko ndani ya Serikali ya Muungano, ndiyo msimamizi mkuu wa vyanzo vya mapato vya Muungano. Mapato hayo ya vyanzo vya Muungano, ambayo yanapaswa kutumika kugharimia shughuli za Muungano pekee na kiasi kinachobaki kikipaswa kugawanywa kwa washirika kwa ajili ya maendeleo, hayatumiki yote kwa lengo hilo.
Kwa miaka mingi sasa, kiasi cha mapato yatokanayo na vyanzo vya Muungano ambacho kimekuwa kikitumika kugharimia shughuli za Muungano ni chini ya 35% tu ya mapato yote, na hivyo, Zanzibar inaituhumu Tanzania Bara, kwamba kiasi kinachobaki cha 65% hutumika kwa shughuli za maendeleo zisizo za Muungano za upande wa Tanzania Bara. Huu ndio msingi mkuu wa madai ya Tanzania Bara kunufaika na ‘koti la Muungano’.
Tanzania Bara, ambayo iko ndani ya Serikali ya Muungano, ndiyo msimamizi wa Sera za Nje za Taifa na ndiye Mwakilishi wa Tanzania kwenye vyombo mbalimbali vya kimataifa.
Kwa kutumia nafasi hii, Tanzania Bara, imekuwa ikipata mikopo na misaada kutoka nje kwa niaba ya washirika wote wawili, lakini misaada hiyo na mikopo imekuwa ikitumika zaidi katika miradi ya maendeleo ya Tanzania Bara.
Kwa kutumia fursa hii, Tanzania Bara, katika ‘koti la Muungano’, imeweza kuingia katika taasisi mbalimbali za kimataifa Kama SADC; EAC; FIFA; WHO; UNESCO nk, na manufaa ya ushiriki wa Tanzania kwenye taasisi hizo yamekuwa hayagawanywi kwa usawa baina ya washirika wote wa Muungano.
Tanzania Bara, ambayo iko ndani ya Serikali ya Muungano, ndiyo msimamizi mkuu wa fedha, sera za uchumi na utumishi katika Wizara za Muungano. Kwa kutumia nafasi hiyo, Tanzania Bara imekuwa haigawi sawia manufaa ya ajira na fedha kwenye taasisi hizo. Zanzibar, bila kujali hali yake halisi ya udogo kieneo na uchache wa wakaazi, inadai manufaa ya Muungano kama ajira, yagawiwe sawa baina ya Washirika hao wawili.
Kwa matazamo wa Zanzibar, ajira kwenye taasisi za Muungano kama uteuzi wa mabalozi nje, ajira katika vyombo vya ulinzi na usalama vinapaswa vigawiwe sawa!
Aidha, manufaa ya kifedha kama scholarships na mikopo ya wanafunzi wa elimu ya juu yanapaswa yagawanywe kwa washirika wote wawili kwa usawa!
Aidha, uongozi katika taasisi za Muungano kama nafasi za waziri, katibu wakuu, wakurugenzi na wakuu wa vyombo vya ulinzi na usalama utolewe kwa kupokezana baina ya Tanzania Bara na Zanzibar.
Tanzania Bara, ambayo iko ndani ya koti la Muungano, ndiyo msimamizi na mtungaji wa sera nyingi za kijamii kwa Tanzania, kwa kutumia fursa hiyo, Tanzania Bara imekuwa ikiinyima Zanzibar uhuru wa kujiamulia mambo yake ya kijamii na kiimani.
Upande wa Tanzania Bara, unaituhumu Zanzibar kunufaika na ‘kudai manufaa zaidi’ kutokana na Muungano, wakati huo huo kuendelea kuomba ‘isiwajibike’ kuchangia Muungano kwa kuwa uchumi wake eti ni mdogo’, kinyume na ukweli halisi kwamba Zanzibar inaeneo dogo (2,600km2, sawa na Jimbo la Uchaguzi la Mwibara, Bunda!) na watu wachache (watu 1,300,000 tu), sawa na wakazi wa Wilaya mbili za Mkoa Shinyanga za Kahama na Shinyanga)!
Baadhi ya Mifano ya manufaa hayo ‘yaliyopita kiasi’ kwa Zanzibar kwa muono wa Tanzania Bara ni yafuatayo:-
Zanzibar, ambayo ni sehemu ya Tanzania yenye wakazi 1,300,000 (sawa na 3% ya Watanzania wote ambao ni 45,000,000), ina wabunge zaidi ya 80 kwenye Bunge la Muungano lenye wabunge 357!
Wabunge hawa, ambao wanalipwa zaidi ya Tshs 10bn kila mwaka kupitia mishahara, posho na marupurupu mengine ukiwamo mfuko wa jimbo, hushiriki kwenye mijadala bungeni ambayo zaidi ya 80% ya mijadala hiyo inahusu Mambo yasiyo ya Muungano ya Tanzania Bara.
Zanzibar, ambayo ni sehemu ya Tanzania, imekuwa na mfumo wake wa utambuzi wa raia wake, na hivyo, kwa sheria yake, kuweza kuwatenga Watanzania Bara kwenye fursa za ajira na umiliki wa ardhi Zanzibar, wakati huo huo wao wakinufaika na fursa hizo upande wa Tanzania Bara.
Zanzibar kiuchumi iko vizuri kuliko Bara, kwani kwa bajeti yake ya Tshs 740bn kwa watu 1,300,000 ni sawa na wastani wa kutenga Tshs 540,000 za kumhudumia kila raia kwa mwaka. Kwa upande wa Tanzania Bara, wastani wa kibajeti kwa raia ni Tshs 330,000 kwa kila raia kwa mwaka, ambayo ni chini kuliko Zanzibar! Pamoja na hali hiyo, Zanzibar imekuwa ikiomba na kusaidiwa na Muungano (ambamo ndani yake imo Tanganyika kwa zaidi ya 90%) kwenye shughuli za kawaida za kimaendeleo.
Kwa kupitia mfumo huu, Zanzibar imefanikiwa kufanya yafuatayo:-
Kutoa huduma za afya bure, wakati Tanzania Bara haifanyiwi hivyo, kutoa elimu ya masingi hadi sekondari bure, wakati Tanzania Bara haifanywi hivyo, kufikia malengo ya kuunganisha wilaya zote 10 na kata zote za Zanzibar kwa Barabara za Lami, wakati Tanzania Bara wilaya zilizounganishwa kwa lami ni kama 70% tu, kufikisha huduma ya maji salama kwa Wanzanzibari kwa uwiano wa kila kaya tatu kuwa na bomba la maji, kuwezesha kujenga hospitali nzuri za kisasa za wilaya na mikoa wakati Tanzania Bara wilaya na mikoa yenye hospitali za wilaya na mikoa ni 60%, kufikisha huduma ya umeme kwenye kata zote za Zanzibar, kuondoa kabisa tatizo la madawati mashuleni.
Zanzibar, ambayo ni ndogo na ni sehemu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, imekuwa ikitoa viongozi na watumishi kwenye wizara zisizo za Muungano. Mfano, mawaziri kadhaa kutoka Zanzibar wanaongoza wizara zisizo za Muungano.
Zanzibar kubaki na utambulisho wake, kama vile Bendera, Wimbo wa Taifa, Rais, Baraza lake la Wawakilishi, wakati Tanzania Bara imepoteza vyote hivyo kupitia Muungano.
Kwa kuwa Tanzania Bara iko ndani ya Serikali ya Muungano, mapato yake kutokana na rasilimali zake lukuki kama madini, gesi nk zinaingizwa kwenye mfuko mkuu wa Muungano, na hivyo kunufaisha washirika wote, wakati rasilimali za Zanzibar si za Muungano na hukusanywa na serikali ya Zanzibar na kutumika Zanzibar pekee.
Hali hii inaleta ule usemi maarufu kwa Watanzania Bara kwamba kuwalenga Wazanzibari kwamba ‘chetu, chao; na chao, chao’!
Kuvipa hadhi sawa vyombo vya Utawala, Utungaji Sheria na Utoaji Haki vya Muungano na Zanzibar, jambo ambalo si sawa. Kwa mfano, katika maeneo yafuatayo:-
Katika majadiliano ya kuondoa kero za Muungano, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano hukutana na Makamu wa Pili wa Zanzibar, ambaye ki hadhi, si saizi yake. Hii ni kushusha hadhi ya Waziri Mkuu.
Rais wa Jamhuri ya Muungano hulazimika kushauriana na Rais wa Zanzibar katika mambo mengi ya utawala, mfano, katika uteuzi wa wajumbe wa Tume ya Katiba na hata wajumbe wa Bunge la Katika, wakati Rais wa Muungano ni mkubwa kwa wa Zanzibar.
Aidha, Rais wa Muungano huwa nyuma kiitifaki kwa Rais wa Zanzibar kwenye Sherehe za Mapinduzi ya Zanzibar, wakati Zanzibar ni sehemu ya Tanzania.
Spika wa Bunge la Muungao kupewa hadhi iliyo sawa kiitifaki na Spika wa Baraza la Wawakilishi, wakati wawili hawa hawana hadhi sawa, kwani Spika wa Muungano ni wa wote (Bara na Zanzibar).
Mwanasheria Mkuu wa Muungano kupewa hadi sawa na Mwanasheria MKuu wa Zanzibar, na mifano mingine mingi.
Tume imependekeza nini katika haya kwenye Rasimu ya Katiba?
Ili kurekebisha matatizo haya, Tume ya Marekebisho ya Katiba, imependekeza kuunda mfumo mpya wa muungano wa shirikisho, la serikali tatu, ambazo mipaka yake ya kiutendaji itakuwa wazi zaidi.
Katika Ibara ya 1 ya Rasimu ya Katiba, imependekezwa kwamba Tanzania itambuliwe kuwa ni Shirikisho.
Katika sura ya 6 ya Rasimu ya Katiba, mgawanyo huu wa serikali tatu umeelezewa katika ibara kama ifuatavyo:-
Ibara ya 60, inaelezea kuwa Muundo wa Muungano utakuwa wa serikali tatu, za Muungano, Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na Serikali ya Tanganyika. Aidha, ibara hiyo inaanzisha Bunge na Mahakama za Muungano na za Tanganyika. Hii inaivua rasmi Tanganyika ‘koti la Muungano’. Ibara ya 62(3), inaruhusu serikali ya Muungano kusaidia serikali yoyote baina ya ile ya Tanganyika na ile ya Zanzibar kama itahitajika na kuombwa hivyo. Hii inaweka uhalali wa pande zote mbili za Muungano kusaidiwa na serikali ‘ya pamoja, yaani ya Muungano’.
Ibara ya 64 inazitambua Nchi Washirika na majukumu yake. Hivyo, kuweka mipaka ya kiutendaji iliyo wazi baina ya Tanganyika, Zanzibar na Muungano. Aidha, ibara ya 64(5), inaweka wazi kuwa Nchi Washirika zitakuwa na ‘hadhi na haki’ SAWA ndani ya muungano. Ibara hii, kwa kutoweka matakwa ya ‘wajibu sawa kwa washirika, na kuweka usawa wa Haki na Hadhi pekee’, inatoa fursa kwa mbia mmoja, hasa Tanganyika kulalamika kwani, kwa vyovyote vile kwa kuzingatia hali halisi ya ukubwa na wingi wa rasilimali Bara, basi Tanganyika ITAWAJIBIKA ZAIDI, lakini Washirika hawa wawili watapata HAKI na HADHI SAWA!! Hii ni kasoro kubwa katika rasimu kwenye eneo hili.
Ibara ya 65, inaweka Mamlaka ya Washirika kwa maeneo yao, lakini pia kuweka misingi ya HAKI na USAWA katika ushirikiano baina ya Washirika. Aidha, kila mshirika anaruhusiwa kuanzisha mashirikiano na nchi au taasisi za nje kivyake, hii inaondoka malalamiko ya Zanzibar kwamba Tanganyika inanufaika peke yake kupitia mashirikiano hayo!
Mapendekezo ya walio wengi katika Bunge Maalumu la Katiba
Wajumbe walio wengi katika Bunge Maalumu la Katiba, wamependekeza mfumo wa serikali mbili, kwa kufanya hivyo, walio wengi wamependekeza marekebisho kwenye rasimu kama ifuatavyo:-
Bila kusisitiza msingi wa Usawa katika HADHI na HAKI baina ya Washirika wa Muungano, Serikali zitakazokuwepo Mbili za Muungano na ya Zanzibar zitakuwa na ushirikiano. Ibara ya 60 inapendekezwa kuwapo serikali mbili za Muungano na Zanzibar.
Ibara hiyo pia inapendekeza kuanzishwa kwa Bunge na Mahakama za Muungano na Zanzibar. Hata hivyo, Ibara hii, bado haijaainisha UTOFAUTI WA HADHI NA HAKI baina ya vyombo hivyo. Kwa pendekezo hili, bado viongozi wa mihimili ya Dola toka Zanzibar wataendelea kuwa na hadhi sawa na wale wa Muungano, jambo ambalo ni kero, hasa upande wa Bara.
Ibara ya 62 ya mapendekezo ya walio wengi, inaweka misingi ya ushirikiano baina ya Serikali ya Muungano na Serikali ya Zanzibar.
Aidha, ibara ya 62(2), inaelekeza kwamba ‘serikali ya Muungano’ itaisaidia Zanzibar kwenye mambo ya maendeleo yasiyo ya Muungano ili kuleta uwiano wa kimaendeleo katika pande mbili za Muungano.
Pendekezo hili, pamoja na kutotambua ukweli kwamba Zanzibar tayari ‘iko vizuri kimaendeleo kuliko Bara’ hasa kwa sababu ya udogo wake, bado linaweka misingi ya Zanzibar kusaidiwa, tena bila kuweka uwezekano wa Muungano kusaidiwa na Zanzibar, jambo ambalo linawezekana kabisa, kwani endapo Zanzibar ikapata mafuta kwa mfano, kwa udogo wake, uchumi wake unaweza kuimarika ghafla na hivyo kuwa na uwezo wa kusaidia Bara na hata Muungano.
Kwa kuweka msingi wa ‘msaada kwa Zanzibar pekee toka Muungano, ambayo kimsingi ni Bara, tayari linaleta ‘kero kwa siku za usoni kwani Zanzibar haijahitajika kikatiba kusaidia Bara hata pale mambo yake yatakapokuwa safi, ingawa hata sasa yako safi!
Kwa ampendekezo ya walio wengi, Ibara ya 65 inatoa Uhuru kwa Zanzibar kujiunga na taasisi za kimataifa na hivyo kupata misaada na mikopo kwenye maeneo yasiyo ya muungano. Pamoja na uzuri wa jambo hili katika kupunguza malalamiko kwa Zanzibar, ibara hii inaweza kutoa mwanya kwa Zanzibar kuendelea kujitambulisha kimataifa kama nchi, hali inayoweza kutumika hapo baadaye kuifanya Zanzibar kutaka kuwa mwanachama wa UN, walau kama mtazamaji (observer) kama ilivyo Palestine. Jambo hili linahitaji kuangaliwa kwa umakini.
Maoni ya Mwandishi
Kwa maoni yangu, napendekeza, mfumo wa serikali mbili ambao wengi wamependekeza uendelee, lakini unahitaji kuboreshwa zaidi katika maeneo yafuatayo:-
Haki, hadhi na wajibu usiwe sawa bali uwe wa uwiano
Kwa ujumla, walio wengi wamependekeza kuendelea kwa Muundo wa Serikali Mbili, hata hivyo, bado masuala ya HAKI, WAJIBU na HADHI katika kuhudumia na kunufaika na Muungano ambayo ndiyo msingi wa malalamiko mengi yanahitaji kuboreshwa zaidi.
Ni vema kwa wakati huu, tukaweka misingi ushirikiano inayotambua ukweli kwamba Zanzibar ni ndogo, na hivyo ipate WAJIBU, HAKI na HADHI kidogo kuliko Tanzania Bara. Si sawa, kwa mfano, kutoa fursa za ajira kwa usawa. Kutoa fursa za malipo ya mikopo ya elimu ya juu kwa usawa.
Kwa kutambua hali ya Zanzibar, inaweza kufaa kuipa mgao wa wajibu unaolingana na uwezo wake na huo ndio uwe msingi wa Haki kwa ZANZIBAR. Jambo hili liwekwe bayana kwenye KATIBA.
Kama Zanzibar inachangia, kwa mfano, 25% ya mapato ya Muungano, basi ipate haki katika ajira na fedha kwa uwiano huo.
Aidha, kwa kuwa ardhi si suala la Muungano, basi raia wa Tanzania wanaotokea Zanzibar, wapate hadhi tofauti na wale wa Tanzania Bara katika kupata na kumiliki ardhi Bara. Kwa hali ilivyo sasa, ardhi ya Tanzania Bara ni ya Muungano, wakati ile ya Zazibar ni ya Wazanzibar, na hii ni kero!
Namna nyingine ya kurekebisha suala hili la ardhi ni kufanya ardhi kuwa suala la Muungano, na hii itatoa fursa zaidi kwa Wazanzibari kuhamia Bara pale ardhi Zanzibar itakapokuwa imekwisha, lakini wakati huo huo, Wabara wenye uwezo waweze kupata ardhi Zanzibar, na kwa kuwa Zanzibar ardhi ni ndogo, basi hakika bei yake itakuwa ni kubwa na hivyo Wazanzibari wataweza kuuza ardhi yao kwa bei ya juu na kuja kununua ardhi Bara bila vikwazo kwa upande wowote. Hili limetokea kwa Wazaramo wa Kariakoo bila matatizo yoyote.
Aidha, ni muhimu kupata namna ya kuweka hadhi ya Muungano na vyombo vyake vya Dola kuwa kubwa kuliko ile ya Zanzibar. Kwa mfano, kutomlinganisha Spika wa Muungano na Spika wa Zanzibar; Kutomuweka Rais wa Muungano, kwa namna yoyote na mazingira yoyote, kuwa nyuma au sawa kiitifaki na Rais wa Zanzibar; Kutomuweka Waziri Mkuu wa Muungano sawa na Waziri Kiongozi au Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar nk.
Kuwepo Misingi ya Kusaidiana kwa pande mbili
Ni vema pia kutambua misingi iliyoko kwenye Hati ya Muungano, na hivyo, kutokuweka kwenye Katiba ulazima wa Zanzibar kusaidiwa na Bara au Serikali ya Muungano kwenye mambo yasiyo ya Muungano.
Namna nyingine ya kulifanya jambo hili, kama ni lazima, basi ni kuweka msingi wa KUSAIDIANA kwa wote (Zanzibar, Bara na Muungano), kwani hali za kiuchumi zinabadilika na kwa kuwa, Katiba tunayoiandika ni ya kudumu, hata miaka 100, na hivyo kuwapo uwezekano kwa ‘mnyonge/masikini’ sasa kuwa tajiri kesho, jambo linaloweza kuleta mgogoro hapo baadaye kwa kuwa litakuwa ni la kikatiba.
Kuwepo na mabunge mawili katika Bunge la Jamhuri ya Muungano
Ili kuwatendea haki Watanzania Bara wakati wa kujadili mambo ya Bara yasiyo ya Muungano na kupunguza gharama, ni vema Bunge la Muungano likawa na sehemu mbili, za Bunge la Juu na la Chini.
Bunge la Juu, ambalo linaweza kuitwa senate, liwe ni la Muungano. Liwe Bunge Dogo lenye viongozi wawakilishi wenye uzoefu na elimu ya juu na lizungumzie mambo makubwa ya Kitaifa na kusimamia Wizara na Masuala ya Muungano. Mawaziri wa Wizara za Muungano wawajibike huko. Liwepo pia Bunge la Chini litakaloshughulikia mambo ya Tanzania Bara yasiyo ya Muungano.
Bunge hili linaweza kuwa kubwa zaidi ya lile la senate kwa kutambua ukubwa na wingi wa watu Tanzania Bara. Mawaziri wa wizara zisizo za Muungano wawajibike katika Bunge hili.
Muungano wa SERIKALI MBILI uwe “sera ya Taifa”, si sera ya chama kimoja cha siasa
Uzoefu katika mchakato huu wa Katiba unaoendelea umeonyesha na kuchocheya mgawanyiko mkubwa baina ya Watanzania, kati ya wale wanaounga mkono Mpendekezo ya Tume ya ‘’Muungano wa shirikisho la serikali tatu’’ na mpendekezo ya CCM ya ‘’Muungano wa serikali mbili’’.
Msingi wa mapendekezo ya CCM, bila kujali uwezo wa mfumo huo wa serikali mbili kutatua kero za Muungano, ni imani kwamba Muungano wa serikali mbili utalinda Muungano na ni matakwa ya Hati ya Muungano iliyosainiwa na Waasisi wa Taifa hili mwaka 1964. Aidha, kwa kuunganishwa kwa vyama vya TANU na ASP mwaka 1977 na hivyo kuzaliwa kwa CCM, serikali mbili imeendelea kuwa SERA muhimu ya CCM.
Maelezo haya kuwa Muungano wa serikali mbili ndiyo sera ya CCM yamekuwa yakisemwa na viongozi kila wakati, na yalipata kusikika sana mwaka 1993 pale Zanzibar ilipojiunga na OIC na hivyo kupelekea wabunge 55 wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wanaotokea Tanzania Bara, kudai kuundwa kwa serikali ya Tanganyika ndani ya Muungano.
Madai hayo ya wabunge yalizimwa na Mwalimu Nyerere, kwa hoja kwamba serikali mbili si SERA YA CCM na hivyo kwa ukali kabisa, Mwalimu katika kitabu chake cha ‘Uongozi wetu na Hatima ya Tanzania’, kilichochapishwa mwaka 1994, akawataka wasiounga mkono SERA HIYO YA CCM, basi waondoke CCM.
Msimamo huo umeendelea kuwa moja ya sera muhimu ya CCM.
Hata hivyo, kwa uzoefu wa nchi mbalimbali duniani zenye mfumo wa vyama vingi, masuala muhimu kama Sura ya Nchi (ikimaanisha, eneo la nchi, mipaka yake, kuwepo kwa desturi na makabila mbalimbali miongoni mwa raia wa nchi); Muundo wa Serikali na Dola; Sera za Nje za Nchi na Sera za Kiuchumi (kama ni kibepari au ujamaa) huwa ni TUNU za mataifa hayo, na hivyo, hakuna chama kinachoyahodhi au hakuna chama kinachoweza kuyabadilisha au kutoyaweka katika sera zake.
TUNU ZA TAIFA hazibinafsishwi kwa itikadi za kisiasa, kidini, kikanda au kwa kundi lolote dogo ndani ya jamii ya Taifa husika.
Ni kwa msingi huu, mataifa kama Uingereza, Marekani, India, Australia nk, ambayo ni ya Shirikisho lakini yenye demokrasia ya vyama vingi, hakuna chama kinachoweza kuanzishwa na kushinda katika uchaguzi katika mataifa hayo kwa sera za kubadilisha mambo hayo.
Uingereza imeendelea kuwa UNITED KINGODOM, bila kujali chama kinachoshinda uchaguzi kama ni Labour, au Conservative au chama kingine.
Marekani imeendelea kuwa taifa la shirikisho la UNITED STATES OF AMERICA bila kujali kama ni Democrats au Republican walioshinda.
Kuna mataifa kama ISRAEL, yameweka hata LUGHA ya Taifa na makao makuu ya nchi kama mambo ambayo ni TUNU ZA TAIFA ambazo hazibadiliki kutokana na vyama vya siasa.
Katika katiba yake, Israel imesema, “… Israel is a sovereign Jewish Republic, whose Headquaters shall be UNDIVIDED JERUSALEM…”. Na imeendele kuwa hivyo kwa kuheshimiwa na kulindwa na vyama vyote vya Siasa.
Ili kufikia hatua hiyo ya kupata TUNU na SERA ZA KITAIFA mataifa hayo yalifanya hivyo kwa njia ya KURA YA MAONI KWA WANANCHI WAKE WOTE.
Hivyo, ni vema, suala kama UWEPO WA MUUNGANO na MUUNDO WAKE, likaamuliwa na wananchi wote kwa NJIA YA KURA YA MAONI, na kisha litakavyokubaliwa, litakuwa ni SERA YA TAIFA na si sera ya chama kimoja cha siasa.
Kwa mfumo tulionao wa siasa ya vyama vingi na kwa kufanya suala la muungano wa SERIKALI MBILI kuwa ni sera ya CCM, basi tunaliweka jambo hili muhimu katika hatari ya kupotea siku CCM itakapoondoka madarakani.
Kwa kutambua uwepo wa vyama vingi na uwezekano wa vyama hivyo kushinda siku moja, ndiyo maana Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ilifanyiwa marekebisho mwaka 1992 kwa kumfanya Rais wa Zanzibar asiwe makamu wa Kwanza wa Rais wa Muungano, badala yake, awepo MGOMBEA MWENZA wa urais ambaye atatoka upande wa pili wa Muungano.
Mabadiliko haya, kwa wahafidhina, walipaswa kuyakataa kwani, Hati ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 1964 ilianzisha nafasi ya Makamu wa Wawili wa Rais, na ilikuwa hivyo tangu 1964 hadi 1992.
Mabadiliko hayo ya Katiba ya mwaka 1992, yalikuwa pia ni fursa ya kuweza kuweka mabadiliko mengine ya kulinda Muungano na Muundo wake wa SERIKALI MBILI kuwa TUNU ZA TAIFA na si SERA YA CHAMA KIMOJA.
Kwa kuwa fursa hiyo ya mwaka 1992 haikutumika, basi fursa tuliyonayo sasa, na haina budi itumike ili kutouweka Muungano na muundo wake kwenye mashaka ya kuvunjika kwa kuwa eti tu CCM imeshindwa katika uchaguzi.
Kufanyika kwa jambo hili pia kutafanya sera hii ikubalike na Watanzania wote. Kwa hali ilivyo sasa, hata kama SERA YA MUUNGANO WA SERIKALI MBILI NI NZURI, vyama vya siasa tofauti na CCM vitaipiga vita kwa kuwa ni SERA YA ADUI YAO KISIASA!!
Mchakato huu umetokana na malalamiko kutoka kwa watu kadhaa kuwa Katiba, ambayo imelilea Taifa tangu mwaka 1962, imezeeka, imejaa viraka na hivyo iandikwe upya.
Baada ya kauli ya Rais Jakaya Kikwete ya Desemba mwaka 2011 kwamba angeanzisha mchakato wa kuandika upya Katiba, Bunge lilitunga Sheria ya Mabadiliko ya Katiba, sura 83 mwaka 2012 na mchakato ukaanza kwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba kukusanya maoni na kuwasilisha Rasimu ya pili ya Katiba bungeni mapema Machi, 2014.
Bunge Maalumu la Katiba sasa linaendelea na vikao vyake Dodoma. Mjadala mkali umezuka na unaedelea, kuhusu muundo wa serikali baada ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba kupendekeza kuundwa kwa shirikisho la serikali tatu, kinyume na Katiba ya sasa (Katiba ya mwaka 1977) yenye serkiali mbili.
Je, Katiba yetu imezeeka na hairekebishiki?
Japo swali hili halina umuhimu tena kwa sasa kwani mchakato wa kuandika Katiba mpya unaendelea, mazingira na mijadala inavyoendelea inalazimu wadadisi kurejea swali hili.
Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania iliandikwa mwaka 1977, miaka 37 iliyopita. Tangu wakati huo, imefanyiwa marekebisho kwa nyakati na sababu tofauti mara 14. Katiba hii iliandikwa baada ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar mwaka 1964 ambapo ilikubaliwa kwamba Katiba ya Jamhuri ya Tanganyika ya mwaka 1962 ifanyiwe marekebisho ili kuipa sura ya Muungano na kuifanya kuwa Katiba ya Mpito.
Marekebisho hayo yalifanyika mwaka 1965 na hivyo kuifanya Katiba ya mpito hadi mwaka 1977 ilipoandikwa Katiba ya Kudumu inayotumika hadi hivi sasa.
Tanzania, ambalo ni Taifa la Muungano wa Nchi Mbili za Tanganyika na Zanzibar, ni Taifa changa kwani lina umri wa miaka 50 tu. Ziko nchi zenye umri zaidi ya Taifa letu ambazo zimeendelea kutumia na kurekebisha katiba zao.
Marekani, kwa mfano, inatumia katiba yenye umri wa zaidi ya miaka 200 na ambayo imefanyiwa marekebisho zaidi ya mara 100.
India, kwa upande wake, iliandika katiba yake ya Uhuru mwaka 1945, miaka 70 iliyopita, mwaka 2012 iliifanyia marekebisho katiba yake, marekebisho ya 94 Katika yake hiyo ya mwaka 1945.
Hivyo, madai kwamba Katiba yetu ya sasa imezeeka na kujaa viraka (kwa kufanyiwa marekebisho mara 14) na hivyo iandikwe mpya ni madai yanayoacha mjadala.
Msingi wa malalamiko kuhusu Katiba ya sasa (ya Mwaka 1977)
Kwa mujibu wa taarifa na nyaraka mbalimbali zilizoambatishwa na Rasimu ya pili ya Katiba ‘mpya’ iliyowasilishwa bungeni na Jaji Warioba, Machi 2014, madai ya kuandikwa upya kwa Katiba yetu ni kwamba;
Muungano, ambao umedumu kwa mika 50 sasa, umeghubikwa na malalamiko mengi kutoka kila upande, hasa Zanzibar kulalamika kwamba Tanzania Bara, inanufaika zaidi kiuchumi kwa kuwa Serikali ya Tanzania Bara ndiyo hiyo hiyo ya Muungano wa Tanzania, na hivyo, Bara ‘kuvaa koti la Muungano’.
Madai hayo ya Zanzibar, yameufanya upande huo wa Muungano kuwa na majaribio na maombi ya mara kwa mara ya kudai ‘uhuru zaidi’, hasa kwa lengo la upande huo kunufaika zaidi kiuchumi na kijamii na mahusiano ‘ya nje’.
Kwa upande wa Bara, malalamiko machache yaliyopo ni kwamba ‘upande wa Zanzibar unanufaika zaidi na fursa na faida za Muungano’, wakati huo huo, kutokana na mazingira yake (ya udogo kieneo na kwa idadi ya watu), Zanzibar kuchangia kidogo au kutochangia kabisa ‘gharama za Muungano’.
Mabadiliko ya Kisiasa na Kijamii ambapo Katiba ya sasa, licha ya kufanyiwa mabadiliko, kwa mfano, mwaka 1992 kuruhusu Mfumo wa Vyama vingi, bado Katiba imekuwa ni kikwazo kwa vyama vya siasa vya Upinzani kufanya vizuri katika chaguzi kwa madai kwamba Tume ya Uchaguzi, na vyombo vingine vya demokrasia vimebanwa kikatiba kuegemea upande wa chama tawala hasa kwa kuwa viongozi wake wanateuliwa na Rais ambaye ndiye kiongozi wa chama tawala.
Kuwepo kwa umasikini mkubwa miongoni mwa Watanzania, umasikini ambao hauendani na utajiri wa Taifa wa Maliasili; hali inayoashiria kwamba Katiba ya Sasa haijaweka mifumo mizuri ya kusaidia wananchi wanufaike na kuendelezwa na maliasili na utajiri wa asili wa Taifa letu.
Hali hii imeelezewa kusababishwa na mifumo dhaifu ya uwajibikaji wa viongozi; kukoseka kwa dira ya Taifa baada ya Azimio la Arusha kufutwa mwaka 1991 na misingi dhaifu ya Haki za Binadamu.
Ukweli na uhalali wa sababu au madai ya Katiba mpya na jinsi madai hayo yalivyozingatiwa Katika Rasimu ya Pili ya Katiba inayojadiliwa bungeni.
Kama ilivyoelezwa, msingi mmojawapo wa sababu za kuandika upya kwa Katiba ni malalamiko kuhusu ‘manufaa, hasa ya kiuchumi na kijamii’ ya Muungano.
Nitalizungumzia zaidi eneo hili kwa sasa, na maeneo mengine ya ‘uhuru wa tume ya uchaguzi na vyombo vingine vya kukuza demokrasia’ pamoja na eneo la ‘udhibiti na usimamizi wa rasilimali za Taifa kwa manufaa ya wananchi’, nitayazungumzia katika makala zitakazofuata.
Muungano wa Tanzania, na hasa muundo wake, limekuwa ni eneo la mjadala mpana na mkali sana wakati huu wa mjadala wa Rasimu ya Pili kwenye Bunge Maalumu na nje ya Bunge.
Kwa kutambua umuhimu wa Muungano, Bunge la Jamhuri ya Muungano, lilipopitisha Sheria ya Mabadiiko ya Katiba, sura 83, katika kifungu 9(2), liliweka maeneo ambayo yanapaswa kulindwa na kuzingatiwa katika Mchakato na hatimaye kuandikwa kwa Katiba mpya.
Kati ya maeneo hayo, ni uwepo wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.
Katika kufanya kazi yake, Tume ya Mabadiliko ya Katiba, ilizingatia eneo hilo kwa mtazamo kwamba ‘eneo hilo linapaswa kulindwa na kuimarishwa’, na hivyo tume kujipa uhuru wa ‘kupendekeza marekebisho’ ambayo Tume inaamini yataboresha Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Kwa utafiti wa aina za Muungano, Tume inasema, Muungano wa nchi zaidi ya moja huleta ama serikali moja (yaani Muungano uitwao unitary union), au serikali mbili au zaidi (katika mfumo wa shirikisho, yaani federation) au serikali tatu zinazoshirikiana kimkataba (yaani confederation).
Katika aina zote hizo za muungano, bado uwezekano wa muungano kuvunjika upo (bila kujali idadi ya serikali zinazoundwa baada ya muungano).
Kwa maoni ya Tume, uimara wa muungano hautokani na idadi ya serikali zinazoundwa, bali ‘dhamira ya kisiasa’ kusimamia na kumaliza ‘malalamiko kuhusu muungano yanayotoka kwenye nchi washirika’.
Kwa tafsiri hiyo ya kifungu hicho cha sheria, Tume, kwa kuamini kwamba inaboresha na kwa kuzingatia tafiti kadhaa ambazo ilifanya na kwa kusikiliza maoni ya wananchi kadhaa kuhusu jambo hilo (la Muungano) na kwa kutambua hatua ambazo zimekuwa zikichukuliwa na upande mmoja wa Muungano, hususan Zanzibar kujitafutia ‘uhuru zaidi’ (hasa kupitia marekebisho ya 10 ya Katiba ya Zanzibar ya Mwaka 1984 yaliyofanywa mwaka 2010) , ilipendekeza ‘kuivua Tanzania Bara koti la Muungano’, na hivyo kupendekeza kuwepo kwa serikali ya ‘kati au ya Ushirika au ya Washirika wote wawili’, serikali ya Tatu, ya Shirikisho, sambamba na ile ya Tanganyika inayoanzishwa kutoka Tanzania Bara iliyokuwa ndani ya Muungano.
Utafiti wa tume kwa nchi mbalimbali zilizoungana, unaonyesha kwamba, ipo miungano iliyodumu ya serikali moja, na mingine ya serikali mbili au zaidi (yaani ya shirikisho), na pia ipo mifano ya nchi zilizokuwa za muungano zilizokuwa za serikali moja na nyingine zaidi ya serikali mbili ambazo miungano yao imevunjika.
Hii inathibitisha ukweli kwamba, idadi ya serikali pekee, hailindi muungano. Nchi za Somalia (Somalia na Somaliland); Ethiopia (Ethiopia na Eritrea), Sudan (Sudan Kusini na Kaskazini) zote zilikuwa na muungano wa serikali moja (unitary union), lakini miungano hiyo imevunjika.
Zipo pia nchi za shirikisho, kama Urusi (USSR), Chekoslovakia na Yugoslavia zilizokuwa za shirikisho nazo zimesambaratika! Aidha, zipo nchi zenye mashirikisho (serikali zaidi ya moja) ambazo zinaendelea kudumu kama vile Canada, India, Brazil, Marekani na hata Ujerumani.
Kwa hiyo, kwa maoni ya Tume, dawa ya kulinda muungano wetu ni kubadilisha muundo wa muungano huo kutoka muundo wa serikali mbili wenye malalamiko lukuki yasiyokoma, na kuunda shirikisho la serikali tatu ambazo mipaka yake ya kiutendaji inaeleweka vizuri.
Kwa mtazamo wa Tume na baadhi ya watu, kuitenganisha Serikali ya Tanganyika na Serikali ya Muungano, kutapunguza malalamiko, hasa kutoka upande wa Zanzibar kwamba Tanganyika imevaa koti la Muungano na hivyo kunufaika zaidi kiuchumi na Muungano.
Malalamiko ya Zanzibar, ambayo yamekuwa kichocheo kwa mshirika huyo katika Muungano kuchukua hatua za ‘kujitafutia uhuru zaidi’ na hivyo kunufaika zaidi kiuchumi, yasiporekebishwa yanaweza kusababisha Muungano kuvunjika, jambo ambalo Tume imeagizwa kisheria kwamba iweke mazingira ya kuzuia lisitokee.
Hali ya Muungano ikoje kwa sasa, nani ananufaika zaidi?
Ukiuliza swali hili kwa kila upande wa Muungano, kila upande utasema upande mmoja unanufaika zaidi. Tuanze na upande mmoja baada ya mwingine.
Upande wa Zanzibar unatuhumu Bara kunufaika zaidi hasa kwa misingi ifuatayo:-
Tanzania Bara, ambayo iko ndani ya Serikali ya Muungano, ndiyo msimamizi mkuu wa vyanzo vya mapato vya Muungano. Mapato hayo ya vyanzo vya Muungano, ambayo yanapaswa kutumika kugharimia shughuli za Muungano pekee na kiasi kinachobaki kikipaswa kugawanywa kwa washirika kwa ajili ya maendeleo, hayatumiki yote kwa lengo hilo.
Kwa miaka mingi sasa, kiasi cha mapato yatokanayo na vyanzo vya Muungano ambacho kimekuwa kikitumika kugharimia shughuli za Muungano ni chini ya 35% tu ya mapato yote, na hivyo, Zanzibar inaituhumu Tanzania Bara, kwamba kiasi kinachobaki cha 65% hutumika kwa shughuli za maendeleo zisizo za Muungano za upande wa Tanzania Bara. Huu ndio msingi mkuu wa madai ya Tanzania Bara kunufaika na ‘koti la Muungano’.
Tanzania Bara, ambayo iko ndani ya Serikali ya Muungano, ndiyo msimamizi wa Sera za Nje za Taifa na ndiye Mwakilishi wa Tanzania kwenye vyombo mbalimbali vya kimataifa.
Kwa kutumia nafasi hii, Tanzania Bara, imekuwa ikipata mikopo na misaada kutoka nje kwa niaba ya washirika wote wawili, lakini misaada hiyo na mikopo imekuwa ikitumika zaidi katika miradi ya maendeleo ya Tanzania Bara.
Kwa kutumia fursa hii, Tanzania Bara, katika ‘koti la Muungano’, imeweza kuingia katika taasisi mbalimbali za kimataifa Kama SADC; EAC; FIFA; WHO; UNESCO nk, na manufaa ya ushiriki wa Tanzania kwenye taasisi hizo yamekuwa hayagawanywi kwa usawa baina ya washirika wote wa Muungano.
Tanzania Bara, ambayo iko ndani ya Serikali ya Muungano, ndiyo msimamizi mkuu wa fedha, sera za uchumi na utumishi katika Wizara za Muungano. Kwa kutumia nafasi hiyo, Tanzania Bara imekuwa haigawi sawia manufaa ya ajira na fedha kwenye taasisi hizo. Zanzibar, bila kujali hali yake halisi ya udogo kieneo na uchache wa wakaazi, inadai manufaa ya Muungano kama ajira, yagawiwe sawa baina ya Washirika hao wawili.
Kwa matazamo wa Zanzibar, ajira kwenye taasisi za Muungano kama uteuzi wa mabalozi nje, ajira katika vyombo vya ulinzi na usalama vinapaswa vigawiwe sawa!
Aidha, manufaa ya kifedha kama scholarships na mikopo ya wanafunzi wa elimu ya juu yanapaswa yagawanywe kwa washirika wote wawili kwa usawa!
Aidha, uongozi katika taasisi za Muungano kama nafasi za waziri, katibu wakuu, wakurugenzi na wakuu wa vyombo vya ulinzi na usalama utolewe kwa kupokezana baina ya Tanzania Bara na Zanzibar.
Tanzania Bara, ambayo iko ndani ya koti la Muungano, ndiyo msimamizi na mtungaji wa sera nyingi za kijamii kwa Tanzania, kwa kutumia fursa hiyo, Tanzania Bara imekuwa ikiinyima Zanzibar uhuru wa kujiamulia mambo yake ya kijamii na kiimani.
Upande wa Tanzania Bara, unaituhumu Zanzibar kunufaika na ‘kudai manufaa zaidi’ kutokana na Muungano, wakati huo huo kuendelea kuomba ‘isiwajibike’ kuchangia Muungano kwa kuwa uchumi wake eti ni mdogo’, kinyume na ukweli halisi kwamba Zanzibar inaeneo dogo (2,600km2, sawa na Jimbo la Uchaguzi la Mwibara, Bunda!) na watu wachache (watu 1,300,000 tu), sawa na wakazi wa Wilaya mbili za Mkoa Shinyanga za Kahama na Shinyanga)!
Baadhi ya Mifano ya manufaa hayo ‘yaliyopita kiasi’ kwa Zanzibar kwa muono wa Tanzania Bara ni yafuatayo:-
Zanzibar, ambayo ni sehemu ya Tanzania yenye wakazi 1,300,000 (sawa na 3% ya Watanzania wote ambao ni 45,000,000), ina wabunge zaidi ya 80 kwenye Bunge la Muungano lenye wabunge 357!
Wabunge hawa, ambao wanalipwa zaidi ya Tshs 10bn kila mwaka kupitia mishahara, posho na marupurupu mengine ukiwamo mfuko wa jimbo, hushiriki kwenye mijadala bungeni ambayo zaidi ya 80% ya mijadala hiyo inahusu Mambo yasiyo ya Muungano ya Tanzania Bara.
Zanzibar, ambayo ni sehemu ya Tanzania, imekuwa na mfumo wake wa utambuzi wa raia wake, na hivyo, kwa sheria yake, kuweza kuwatenga Watanzania Bara kwenye fursa za ajira na umiliki wa ardhi Zanzibar, wakati huo huo wao wakinufaika na fursa hizo upande wa Tanzania Bara.
Zanzibar kiuchumi iko vizuri kuliko Bara, kwani kwa bajeti yake ya Tshs 740bn kwa watu 1,300,000 ni sawa na wastani wa kutenga Tshs 540,000 za kumhudumia kila raia kwa mwaka. Kwa upande wa Tanzania Bara, wastani wa kibajeti kwa raia ni Tshs 330,000 kwa kila raia kwa mwaka, ambayo ni chini kuliko Zanzibar! Pamoja na hali hiyo, Zanzibar imekuwa ikiomba na kusaidiwa na Muungano (ambamo ndani yake imo Tanganyika kwa zaidi ya 90%) kwenye shughuli za kawaida za kimaendeleo.
Kwa kupitia mfumo huu, Zanzibar imefanikiwa kufanya yafuatayo:-
Kutoa huduma za afya bure, wakati Tanzania Bara haifanyiwi hivyo, kutoa elimu ya masingi hadi sekondari bure, wakati Tanzania Bara haifanywi hivyo, kufikia malengo ya kuunganisha wilaya zote 10 na kata zote za Zanzibar kwa Barabara za Lami, wakati Tanzania Bara wilaya zilizounganishwa kwa lami ni kama 70% tu, kufikisha huduma ya maji salama kwa Wanzanzibari kwa uwiano wa kila kaya tatu kuwa na bomba la maji, kuwezesha kujenga hospitali nzuri za kisasa za wilaya na mikoa wakati Tanzania Bara wilaya na mikoa yenye hospitali za wilaya na mikoa ni 60%, kufikisha huduma ya umeme kwenye kata zote za Zanzibar, kuondoa kabisa tatizo la madawati mashuleni.
Zanzibar, ambayo ni ndogo na ni sehemu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, imekuwa ikitoa viongozi na watumishi kwenye wizara zisizo za Muungano. Mfano, mawaziri kadhaa kutoka Zanzibar wanaongoza wizara zisizo za Muungano.
Zanzibar kubaki na utambulisho wake, kama vile Bendera, Wimbo wa Taifa, Rais, Baraza lake la Wawakilishi, wakati Tanzania Bara imepoteza vyote hivyo kupitia Muungano.
Kwa kuwa Tanzania Bara iko ndani ya Serikali ya Muungano, mapato yake kutokana na rasilimali zake lukuki kama madini, gesi nk zinaingizwa kwenye mfuko mkuu wa Muungano, na hivyo kunufaisha washirika wote, wakati rasilimali za Zanzibar si za Muungano na hukusanywa na serikali ya Zanzibar na kutumika Zanzibar pekee.
Hali hii inaleta ule usemi maarufu kwa Watanzania Bara kwamba kuwalenga Wazanzibari kwamba ‘chetu, chao; na chao, chao’!
Kuvipa hadhi sawa vyombo vya Utawala, Utungaji Sheria na Utoaji Haki vya Muungano na Zanzibar, jambo ambalo si sawa. Kwa mfano, katika maeneo yafuatayo:-
Katika majadiliano ya kuondoa kero za Muungano, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano hukutana na Makamu wa Pili wa Zanzibar, ambaye ki hadhi, si saizi yake. Hii ni kushusha hadhi ya Waziri Mkuu.
Rais wa Jamhuri ya Muungano hulazimika kushauriana na Rais wa Zanzibar katika mambo mengi ya utawala, mfano, katika uteuzi wa wajumbe wa Tume ya Katiba na hata wajumbe wa Bunge la Katika, wakati Rais wa Muungano ni mkubwa kwa wa Zanzibar.
Aidha, Rais wa Muungano huwa nyuma kiitifaki kwa Rais wa Zanzibar kwenye Sherehe za Mapinduzi ya Zanzibar, wakati Zanzibar ni sehemu ya Tanzania.
Spika wa Bunge la Muungao kupewa hadhi iliyo sawa kiitifaki na Spika wa Baraza la Wawakilishi, wakati wawili hawa hawana hadhi sawa, kwani Spika wa Muungano ni wa wote (Bara na Zanzibar).
Mwanasheria Mkuu wa Muungano kupewa hadi sawa na Mwanasheria MKuu wa Zanzibar, na mifano mingine mingi.
Tume imependekeza nini katika haya kwenye Rasimu ya Katiba?
Ili kurekebisha matatizo haya, Tume ya Marekebisho ya Katiba, imependekeza kuunda mfumo mpya wa muungano wa shirikisho, la serikali tatu, ambazo mipaka yake ya kiutendaji itakuwa wazi zaidi.
Katika Ibara ya 1 ya Rasimu ya Katiba, imependekezwa kwamba Tanzania itambuliwe kuwa ni Shirikisho.
Katika sura ya 6 ya Rasimu ya Katiba, mgawanyo huu wa serikali tatu umeelezewa katika ibara kama ifuatavyo:-
Ibara ya 60, inaelezea kuwa Muundo wa Muungano utakuwa wa serikali tatu, za Muungano, Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na Serikali ya Tanganyika. Aidha, ibara hiyo inaanzisha Bunge na Mahakama za Muungano na za Tanganyika. Hii inaivua rasmi Tanganyika ‘koti la Muungano’. Ibara ya 62(3), inaruhusu serikali ya Muungano kusaidia serikali yoyote baina ya ile ya Tanganyika na ile ya Zanzibar kama itahitajika na kuombwa hivyo. Hii inaweka uhalali wa pande zote mbili za Muungano kusaidiwa na serikali ‘ya pamoja, yaani ya Muungano’.
Ibara ya 64 inazitambua Nchi Washirika na majukumu yake. Hivyo, kuweka mipaka ya kiutendaji iliyo wazi baina ya Tanganyika, Zanzibar na Muungano. Aidha, ibara ya 64(5), inaweka wazi kuwa Nchi Washirika zitakuwa na ‘hadhi na haki’ SAWA ndani ya muungano. Ibara hii, kwa kutoweka matakwa ya ‘wajibu sawa kwa washirika, na kuweka usawa wa Haki na Hadhi pekee’, inatoa fursa kwa mbia mmoja, hasa Tanganyika kulalamika kwani, kwa vyovyote vile kwa kuzingatia hali halisi ya ukubwa na wingi wa rasilimali Bara, basi Tanganyika ITAWAJIBIKA ZAIDI, lakini Washirika hawa wawili watapata HAKI na HADHI SAWA!! Hii ni kasoro kubwa katika rasimu kwenye eneo hili.
Ibara ya 65, inaweka Mamlaka ya Washirika kwa maeneo yao, lakini pia kuweka misingi ya HAKI na USAWA katika ushirikiano baina ya Washirika. Aidha, kila mshirika anaruhusiwa kuanzisha mashirikiano na nchi au taasisi za nje kivyake, hii inaondoka malalamiko ya Zanzibar kwamba Tanganyika inanufaika peke yake kupitia mashirikiano hayo!
Mapendekezo ya walio wengi katika Bunge Maalumu la Katiba
Wajumbe walio wengi katika Bunge Maalumu la Katiba, wamependekeza mfumo wa serikali mbili, kwa kufanya hivyo, walio wengi wamependekeza marekebisho kwenye rasimu kama ifuatavyo:-
Bila kusisitiza msingi wa Usawa katika HADHI na HAKI baina ya Washirika wa Muungano, Serikali zitakazokuwepo Mbili za Muungano na ya Zanzibar zitakuwa na ushirikiano. Ibara ya 60 inapendekezwa kuwapo serikali mbili za Muungano na Zanzibar.
Ibara hiyo pia inapendekeza kuanzishwa kwa Bunge na Mahakama za Muungano na Zanzibar. Hata hivyo, Ibara hii, bado haijaainisha UTOFAUTI WA HADHI NA HAKI baina ya vyombo hivyo. Kwa pendekezo hili, bado viongozi wa mihimili ya Dola toka Zanzibar wataendelea kuwa na hadhi sawa na wale wa Muungano, jambo ambalo ni kero, hasa upande wa Bara.
Ibara ya 62 ya mapendekezo ya walio wengi, inaweka misingi ya ushirikiano baina ya Serikali ya Muungano na Serikali ya Zanzibar.
Aidha, ibara ya 62(2), inaelekeza kwamba ‘serikali ya Muungano’ itaisaidia Zanzibar kwenye mambo ya maendeleo yasiyo ya Muungano ili kuleta uwiano wa kimaendeleo katika pande mbili za Muungano.
Pendekezo hili, pamoja na kutotambua ukweli kwamba Zanzibar tayari ‘iko vizuri kimaendeleo kuliko Bara’ hasa kwa sababu ya udogo wake, bado linaweka misingi ya Zanzibar kusaidiwa, tena bila kuweka uwezekano wa Muungano kusaidiwa na Zanzibar, jambo ambalo linawezekana kabisa, kwani endapo Zanzibar ikapata mafuta kwa mfano, kwa udogo wake, uchumi wake unaweza kuimarika ghafla na hivyo kuwa na uwezo wa kusaidia Bara na hata Muungano.
Kwa kuweka msingi wa ‘msaada kwa Zanzibar pekee toka Muungano, ambayo kimsingi ni Bara, tayari linaleta ‘kero kwa siku za usoni kwani Zanzibar haijahitajika kikatiba kusaidia Bara hata pale mambo yake yatakapokuwa safi, ingawa hata sasa yako safi!
Kwa ampendekezo ya walio wengi, Ibara ya 65 inatoa Uhuru kwa Zanzibar kujiunga na taasisi za kimataifa na hivyo kupata misaada na mikopo kwenye maeneo yasiyo ya muungano. Pamoja na uzuri wa jambo hili katika kupunguza malalamiko kwa Zanzibar, ibara hii inaweza kutoa mwanya kwa Zanzibar kuendelea kujitambulisha kimataifa kama nchi, hali inayoweza kutumika hapo baadaye kuifanya Zanzibar kutaka kuwa mwanachama wa UN, walau kama mtazamaji (observer) kama ilivyo Palestine. Jambo hili linahitaji kuangaliwa kwa umakini.
Maoni ya Mwandishi
Kwa maoni yangu, napendekeza, mfumo wa serikali mbili ambao wengi wamependekeza uendelee, lakini unahitaji kuboreshwa zaidi katika maeneo yafuatayo:-
Haki, hadhi na wajibu usiwe sawa bali uwe wa uwiano
Kwa ujumla, walio wengi wamependekeza kuendelea kwa Muundo wa Serikali Mbili, hata hivyo, bado masuala ya HAKI, WAJIBU na HADHI katika kuhudumia na kunufaika na Muungano ambayo ndiyo msingi wa malalamiko mengi yanahitaji kuboreshwa zaidi.
Ni vema kwa wakati huu, tukaweka misingi ushirikiano inayotambua ukweli kwamba Zanzibar ni ndogo, na hivyo ipate WAJIBU, HAKI na HADHI kidogo kuliko Tanzania Bara. Si sawa, kwa mfano, kutoa fursa za ajira kwa usawa. Kutoa fursa za malipo ya mikopo ya elimu ya juu kwa usawa.
Kwa kutambua hali ya Zanzibar, inaweza kufaa kuipa mgao wa wajibu unaolingana na uwezo wake na huo ndio uwe msingi wa Haki kwa ZANZIBAR. Jambo hili liwekwe bayana kwenye KATIBA.
Kama Zanzibar inachangia, kwa mfano, 25% ya mapato ya Muungano, basi ipate haki katika ajira na fedha kwa uwiano huo.
Aidha, kwa kuwa ardhi si suala la Muungano, basi raia wa Tanzania wanaotokea Zanzibar, wapate hadhi tofauti na wale wa Tanzania Bara katika kupata na kumiliki ardhi Bara. Kwa hali ilivyo sasa, ardhi ya Tanzania Bara ni ya Muungano, wakati ile ya Zazibar ni ya Wazanzibar, na hii ni kero!
Namna nyingine ya kurekebisha suala hili la ardhi ni kufanya ardhi kuwa suala la Muungano, na hii itatoa fursa zaidi kwa Wazanzibari kuhamia Bara pale ardhi Zanzibar itakapokuwa imekwisha, lakini wakati huo huo, Wabara wenye uwezo waweze kupata ardhi Zanzibar, na kwa kuwa Zanzibar ardhi ni ndogo, basi hakika bei yake itakuwa ni kubwa na hivyo Wazanzibari wataweza kuuza ardhi yao kwa bei ya juu na kuja kununua ardhi Bara bila vikwazo kwa upande wowote. Hili limetokea kwa Wazaramo wa Kariakoo bila matatizo yoyote.
Aidha, ni muhimu kupata namna ya kuweka hadhi ya Muungano na vyombo vyake vya Dola kuwa kubwa kuliko ile ya Zanzibar. Kwa mfano, kutomlinganisha Spika wa Muungano na Spika wa Zanzibar; Kutomuweka Rais wa Muungano, kwa namna yoyote na mazingira yoyote, kuwa nyuma au sawa kiitifaki na Rais wa Zanzibar; Kutomuweka Waziri Mkuu wa Muungano sawa na Waziri Kiongozi au Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar nk.
Kuwepo Misingi ya Kusaidiana kwa pande mbili
Ni vema pia kutambua misingi iliyoko kwenye Hati ya Muungano, na hivyo, kutokuweka kwenye Katiba ulazima wa Zanzibar kusaidiwa na Bara au Serikali ya Muungano kwenye mambo yasiyo ya Muungano.
Namna nyingine ya kulifanya jambo hili, kama ni lazima, basi ni kuweka msingi wa KUSAIDIANA kwa wote (Zanzibar, Bara na Muungano), kwani hali za kiuchumi zinabadilika na kwa kuwa, Katiba tunayoiandika ni ya kudumu, hata miaka 100, na hivyo kuwapo uwezekano kwa ‘mnyonge/masikini’ sasa kuwa tajiri kesho, jambo linaloweza kuleta mgogoro hapo baadaye kwa kuwa litakuwa ni la kikatiba.
Kuwepo na mabunge mawili katika Bunge la Jamhuri ya Muungano
Ili kuwatendea haki Watanzania Bara wakati wa kujadili mambo ya Bara yasiyo ya Muungano na kupunguza gharama, ni vema Bunge la Muungano likawa na sehemu mbili, za Bunge la Juu na la Chini.
Bunge la Juu, ambalo linaweza kuitwa senate, liwe ni la Muungano. Liwe Bunge Dogo lenye viongozi wawakilishi wenye uzoefu na elimu ya juu na lizungumzie mambo makubwa ya Kitaifa na kusimamia Wizara na Masuala ya Muungano. Mawaziri wa Wizara za Muungano wawajibike huko. Liwepo pia Bunge la Chini litakaloshughulikia mambo ya Tanzania Bara yasiyo ya Muungano.
Bunge hili linaweza kuwa kubwa zaidi ya lile la senate kwa kutambua ukubwa na wingi wa watu Tanzania Bara. Mawaziri wa wizara zisizo za Muungano wawajibike katika Bunge hili.
Muungano wa SERIKALI MBILI uwe “sera ya Taifa”, si sera ya chama kimoja cha siasa
Uzoefu katika mchakato huu wa Katiba unaoendelea umeonyesha na kuchocheya mgawanyiko mkubwa baina ya Watanzania, kati ya wale wanaounga mkono Mpendekezo ya Tume ya ‘’Muungano wa shirikisho la serikali tatu’’ na mpendekezo ya CCM ya ‘’Muungano wa serikali mbili’’.
Msingi wa mapendekezo ya CCM, bila kujali uwezo wa mfumo huo wa serikali mbili kutatua kero za Muungano, ni imani kwamba Muungano wa serikali mbili utalinda Muungano na ni matakwa ya Hati ya Muungano iliyosainiwa na Waasisi wa Taifa hili mwaka 1964. Aidha, kwa kuunganishwa kwa vyama vya TANU na ASP mwaka 1977 na hivyo kuzaliwa kwa CCM, serikali mbili imeendelea kuwa SERA muhimu ya CCM.
Maelezo haya kuwa Muungano wa serikali mbili ndiyo sera ya CCM yamekuwa yakisemwa na viongozi kila wakati, na yalipata kusikika sana mwaka 1993 pale Zanzibar ilipojiunga na OIC na hivyo kupelekea wabunge 55 wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wanaotokea Tanzania Bara, kudai kuundwa kwa serikali ya Tanganyika ndani ya Muungano.
Madai hayo ya wabunge yalizimwa na Mwalimu Nyerere, kwa hoja kwamba serikali mbili si SERA YA CCM na hivyo kwa ukali kabisa, Mwalimu katika kitabu chake cha ‘Uongozi wetu na Hatima ya Tanzania’, kilichochapishwa mwaka 1994, akawataka wasiounga mkono SERA HIYO YA CCM, basi waondoke CCM.
Msimamo huo umeendelea kuwa moja ya sera muhimu ya CCM.
Hata hivyo, kwa uzoefu wa nchi mbalimbali duniani zenye mfumo wa vyama vingi, masuala muhimu kama Sura ya Nchi (ikimaanisha, eneo la nchi, mipaka yake, kuwepo kwa desturi na makabila mbalimbali miongoni mwa raia wa nchi); Muundo wa Serikali na Dola; Sera za Nje za Nchi na Sera za Kiuchumi (kama ni kibepari au ujamaa) huwa ni TUNU za mataifa hayo, na hivyo, hakuna chama kinachoyahodhi au hakuna chama kinachoweza kuyabadilisha au kutoyaweka katika sera zake.
TUNU ZA TAIFA hazibinafsishwi kwa itikadi za kisiasa, kidini, kikanda au kwa kundi lolote dogo ndani ya jamii ya Taifa husika.
Ni kwa msingi huu, mataifa kama Uingereza, Marekani, India, Australia nk, ambayo ni ya Shirikisho lakini yenye demokrasia ya vyama vingi, hakuna chama kinachoweza kuanzishwa na kushinda katika uchaguzi katika mataifa hayo kwa sera za kubadilisha mambo hayo.
Uingereza imeendelea kuwa UNITED KINGODOM, bila kujali chama kinachoshinda uchaguzi kama ni Labour, au Conservative au chama kingine.
Marekani imeendelea kuwa taifa la shirikisho la UNITED STATES OF AMERICA bila kujali kama ni Democrats au Republican walioshinda.
Kuna mataifa kama ISRAEL, yameweka hata LUGHA ya Taifa na makao makuu ya nchi kama mambo ambayo ni TUNU ZA TAIFA ambazo hazibadiliki kutokana na vyama vya siasa.
Katika katiba yake, Israel imesema, “… Israel is a sovereign Jewish Republic, whose Headquaters shall be UNDIVIDED JERUSALEM…”. Na imeendele kuwa hivyo kwa kuheshimiwa na kulindwa na vyama vyote vya Siasa.
Ili kufikia hatua hiyo ya kupata TUNU na SERA ZA KITAIFA mataifa hayo yalifanya hivyo kwa njia ya KURA YA MAONI KWA WANANCHI WAKE WOTE.
Hivyo, ni vema, suala kama UWEPO WA MUUNGANO na MUUNDO WAKE, likaamuliwa na wananchi wote kwa NJIA YA KURA YA MAONI, na kisha litakavyokubaliwa, litakuwa ni SERA YA TAIFA na si sera ya chama kimoja cha siasa.
Kwa mfumo tulionao wa siasa ya vyama vingi na kwa kufanya suala la muungano wa SERIKALI MBILI kuwa ni sera ya CCM, basi tunaliweka jambo hili muhimu katika hatari ya kupotea siku CCM itakapoondoka madarakani.
Kwa kutambua uwepo wa vyama vingi na uwezekano wa vyama hivyo kushinda siku moja, ndiyo maana Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ilifanyiwa marekebisho mwaka 1992 kwa kumfanya Rais wa Zanzibar asiwe makamu wa Kwanza wa Rais wa Muungano, badala yake, awepo MGOMBEA MWENZA wa urais ambaye atatoka upande wa pili wa Muungano.
Mabadiliko haya, kwa wahafidhina, walipaswa kuyakataa kwani, Hati ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 1964 ilianzisha nafasi ya Makamu wa Wawili wa Rais, na ilikuwa hivyo tangu 1964 hadi 1992.
Mabadiliko hayo ya Katiba ya mwaka 1992, yalikuwa pia ni fursa ya kuweza kuweka mabadiliko mengine ya kulinda Muungano na Muundo wake wa SERIKALI MBILI kuwa TUNU ZA TAIFA na si SERA YA CHAMA KIMOJA.
Kwa kuwa fursa hiyo ya mwaka 1992 haikutumika, basi fursa tuliyonayo sasa, na haina budi itumike ili kutouweka Muungano na muundo wake kwenye mashaka ya kuvunjika kwa kuwa eti tu CCM imeshindwa katika uchaguzi.
Kufanyika kwa jambo hili pia kutafanya sera hii ikubalike na Watanzania wote. Kwa hali ilivyo sasa, hata kama SERA YA MUUNGANO WA SERIKALI MBILI NI NZURI, vyama vya siasa tofauti na CCM vitaipiga vita kwa kuwa ni SERA YA ADUI YAO KISIASA!!
Ezekiel Maige ni Mjumbe wa Bunge la Katiba
Raia mwema
0 comments:
Post a Comment